Friday, January 12, 2007

Hivi kweli taifa linakabiliwa na uhaba wa walimu?

(Pichani Mwl.Ngugi alipolitembelea darasa langu la kiswahili.Umefika wakati kwa serikali ya Tanzania kuwathamini walimu kwani walimu ni funguo za fani anuwai.)

Kama ambavyo haijulikani ni kipi kilitangulia kati ya kuku na yai,hali kadhalika na mimi sijui ni kipi kinatangulia kati ya elimu na maendeleo.Ninachoweza kusema, elimu ni chachu (catalyst) ya maendeleo.Elimu ni neno moja ambalo linabeba maana pana na inayojitosheleza.Wanazuoni mbalimbali walitoa nadharia zao juu ya neno hili.Mathalani Aristoto analifafanua neno elimu kama kitendo cha mtu kuweza kuyafahamu yale asiyokuwa akiyafahamu hapo awali.Aristoto anaendelea kuielezea elimu kama ni kitu ambacho kipo siku zote tangu siku mwanadamu anapozaliwa hadi siku ya kufa.Kimsingi elimu ni chachu ya maendeleo kwa jamii yoyote hapa duniani.
Ili kuweza kutoa elimu bora vinahitajika vitu vikuu vitatu; mosi - miundo mbinu kama vile vyumba vya madarasa, pili -walimu bora na tatu-vitendea kazi kwa ujumla wake.Kwa ujumla tatizo kubwa katika huo utatu ni ukosefu kama si upungufu wa walimu.Hili limekuwa tatizo lisilopatiwa ufumbuzi wa kudumu hapa nchini.Siyo shule za msingi wala sekondari au vyuo vikuu,muziki ni ule ule tu; yaani uhaba kama si upungufu wa walimu.
Ukiondoa miji mikubwa kama vile Dar es Salaam,Mwanza na Arusha na pengine katika kila makao makuu ya mikoa na wilaya ni mifano michache ya sehemu ambazo zinajitosheleza.Kwa upande mwingine hali ni mbaya katika maeneo mengine hususani vijijini. Mathalani shule za sekondari zimefunguliwa na zinaendelea kufunguliwa katika kila kata huku zikiwa hazina walimu wa kutosha na lau kama wapo basi ni chini ya idadi na viwango vinayotakiwa.
Kwa ujumla idadi ya walimu wanaohitimu mafunzo ya ualimu kwa ngazi ya stashahada na shahada ni ya kuridhisha na kama wote wakipatiwa mazingira mazuri ya kufanya kazi katika maeneo mbalimbali yenye upungufu hakika tatizo la upungufu wa walimu linaweza kupatiwa ufumbuzi wa kudumu.
Changamoto kwa wizara ya elimu na mafunzo kwa kushirikiana na wizara za sayansi teknolojia na elimu ya juu na ile inayoshughulikia masuala ya ajira waliangalie suala hili kwa mapana yake ili Tanzania iachane na wimbo wa ukosefu wa walimu katika shule za sekondari zinazomilikiwa na serikali pamoja na zile za wazazi kwa kutoa ajira kwa wahitimu wote wa fani hiyo ikiwa ni sambamba na maslahi mazuri kama zilivyo sekta nyingine hapa nchini. "Ualimu ni kazi bwana na wala sio wito".

1 comment:

Anonymous said...

Kiswahili kinazidi kupata heshima hapa ulimwenguni.Nimefuatilia mahojiano fulani ktk BBC na nikagundua ya kwamba muda si mrefu kiswahili kitakuwa zaidi ya lugha ya Afrika.