Sunday, January 28, 2007

Uzalendo upewe kipaumbele badala ya unazi!

Wawakilishi wa Tanzania ktk ligi ya mabingwa Afrika-Yanga kabla ya ushindi mnono wa 5-1 dhidi ya AJSM ya Comoro. (Picha kwa hisani ya Muhidin Michuzi)
Moja ya sera za serikali ya awamu ya nne chini ya Mh. JK ni kuinua michezo na kwa kuanza mchezo wa mpira wa miguu maarufu kama kandanda ndio umepewa kipaumbele.Kutambulika kwa nchi yetu katika ramani ya kabumbu barani Afrika na ulimwenguni kwa ujumla kutatokana na kuimarika kwa vilabu vyetu.Ili kuwa na timu nzuri ya taifa ni vizuri tukawa na vilabu bora vyenye kufanya vizuri katika mashindano ya kimataifa. Kwa ujumla Yanga na Simba ndio vilabu vikubwa katika soka nchini Tanzania vinavyovuta hisia za mashabiki lukuki. Kuwa mnazi wa Simba au Yanga ni utashi lakini ni vema jambo hili likaenda sanjari na uzalendo unapofika wakati wa mechi za kimataifa. Mathalani mwaka huu Yanga ndio wawakilishi wa nchi yetu katika ligi ya mabingwa Afrika ili-hali Simba ni wawakilishi katika kombe la CUF. Kimsingi umefika wakati sasa kwa mashabiki wa timu za Yanga na Simba kuuvaa uzalendo na kuondoa tofauti za kiushabiki wakati moja ya timu zetu inapokuwa inaliwakilisha taifa letu. Mechi za uwanja wa nyumbani ni mechi muhimu ambazo ni vizuri timu zetu zikazitumia kuvuna ushindi mnono.Kisaikolojia mashabiki wana nafasi yao katika kufanikisha au kuzorotesha ushindi ama kwa kushangilia au kwa kuzomea.Si vema na wala si busara kwa watazamaji wanaoingia uwanja wa taifa kutowashangilia wawakilishi wetu kwa kisingizio cha unazi wa Yanga na Simba. Kwa ujumla timu zetu za Yanga na Simba zina nia na uwezo wa kulitoa kimasomaso taifa letu katika mechi za kimataifa.Wanazi tutoe ushirikiano wa kutosha. Mungu Ibariki Tanzania.

1 comment:

Anonymous said...

Isije ikawa ni nguvu ya soda kwa wanajangwani hao!! Lakini kwa sasa wana kocha mzuri.