Thursday, May 10, 2007

Kama ni urafiki mhh! "hii too much".




Kwa jamii yetu mnyama mbwa anafugwa kwa madhumuni ya kusaidia ulinzi. Ila katika jamii nyingine mnyama huyu ni rafiki mkubwa wa binadamu na anapewa heshima zote za rafiki wa kweli. Kudhihirisha hilo ni kosa kubwa kwa wenzetu hawa kumtaja mnyama huyu kwa kutumia pronoun "it". Huwakilishwa na pronoun sawia kabisa na binadamu. Mathalani mbwa dume ni "he" na mbwa jike ni "she". Huo ni mfano mmoja tu wa heshima apewayo mnyama mbwa. Naamini ipo mingi.

Saturday, May 5, 2007

Ujumbe!

Serikali ya Tanzania imedhamiria kuvitangaza vivutio vilivyopo nchini. Hapa ni siku ujumbe wa Tanzania ulipokitembelea chuo kikuu cha New York kwa ajili hiyo. Timu iliongozwa na Mh. Jumanne Maghembe (Waziri wa maliasili na utalii-wa tatu toka shoto). Pia alikuwepo balozi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa Mh. Mahiga-wa nne toka kulia.

Wednesday, May 2, 2007

Hivi kumbe KIMWI chamtoto kwa MALARIA!


Tarehe 25/4 ilikuwa siku ya malaria. Kama ilivyo kwa malaria kuna siku ya UKIMWI pia. Inasikitisha kwamba nguvu nyingi zinatumika katika kupambana na UKIMWI huku malaria ikishika kasi katika kusababisha vifo vingi kuliko UKIMWI. Kwa ujumla inasikitisha na kusononesha kusikia kwamba MALARIA bado ni namba one killer desease hapa Tanzania. Sanjari na hilo karibu zaidi ya 80% ya wagonjwa wanasumbuliwa na malaria huku wengi wao wakiwa watoto na akina mama wajawazito. Nini kifanyike maana malaria inasababisha vifo vingi?

Saturday, April 28, 2007

Kitu hicho!

Ama hakika Teknolojia inakua kila uchao! Hiki kifaa sijui kinaendaje. Wasiwasi wangu ni pale tu kitakapokwaruzwa kama si kugongwa. "weekend njema".

Inawezakana matunda yameanza!


Ziara ya Shaikh Saud bin Saqral Al Qasimi ambaye ni Naibu mtawala wa Ras al Khaiman inaweza ikafungua milango ktk suala zima la uwekezaji hapa nchini Tanzania. Ras Al Khaiman ni miongoni mwa nchi 7 zinazounda muungano wa EMIRATES. Kiuchumi jumuiya ya EMIRATES wamepiga hatua. Ni vema basi viongozi wetu wajifunze mengi toka kwa kiongozi huyo ili kuinua na hatimaye kukuza uchumi wa nchi yetu. Pengine ziara hii ni mojawapo ya matunda ya ziara za viongozi.

Wednesday, April 25, 2007

Hongera Tanzania kwa kutimiza miaka 43 ya Muungano!

Kila la kheri ktk kusheherekea sikukuu ya Muungano.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tz, Mh JK ni kama vile anamwambia Rais wa Burkina Faso "Muungano wetu hautatetereka, nitaulinda na kuutunza kwa kuuimarisha zaidi"

Wednesday, April 18, 2007

Hivi ulifanyalo ndo hasa ulistahili kulifanya!!!


Pichani baba watoto akiwa makini kutoa maelekezo kwa wanawe wanaojaribu kuchora huku mama yao akitazama. Ni njia thabiti ya kuendeleza vipaji.

Kipaji (ability/talent) ni ile hali ambayo kiasili mtu anakuwa na uwezo au mapenzi ya kufanya jambo fulani. Aghalabu vipaji huonekana tangia utotoni. Kila mtoto huwa anaonyesha kile anachokipenda (interest) kwa kujaribu kukifanya mara kwa mara. Kawaida vipaji vinapaswa kuendelezwa na kukuzwa katika mazingira mazuri. Wawajibikaji wakuu kwa hilo ni wazazi au walezi (care givers). Kwa kufanya hivyo watoto watakuwa kwenye nafasi nzuri ya kuyafanya yale wayapendayo. Kama mtoto anaonyesha mapenzi katika kusakata kabumbu basi ni vema aipate elimu yake katika shule zenye mchepuo wa michezo. Sina uhakika kama hili nilifanyalo ndio hasa nililokuwa nikilipenda tangu utotoni. (sikufuru). Lakini nakumbuka nilikuwa napenda sana kuwa muuza duka na nilikuwa nikiwasumbua sana wazazi wangu kwa hilo. Kwa undani huenda kipaji changu kilikuwa biashara. Katika nchi zilizoendelea suala hili linazingatiwa sana kwa ushirikiano wa wazazi na serikali. Kwa kuhitimisha, napenda nikuulize swali dogo mpenzi msomaji, Je hiyo shughuli yako uifanyayo au hiyo kozi unayosoma ni ile hasa ambayo inaendana na kipaji chako?

Tuesday, April 10, 2007

Bifu sasa limekwisha, "sisi wamoja na tuchape kazi".

Pichani "tusameheane mzee kwa yaliyotokea" Kutoka kushoto ni Mh. Spika Sitta , Mh. W/M Lowasa na Mh. Malima. (Picha na Hilary Bujiku)
Siasa bwana ina mambo yake! Mikwara miiiiingi! Binafsi sikuona sababu ya kulumbana sana na kutumia fedha zilizotumika kwa hoja ya Mh. Malima kuhusu muda unaotolewa na ITV kwa viongozi wa kitaifa dhidi ya ule anaopewa Mwenyekiti mtendaji wa IPP katika taarifa za habari za ITV. Hili lilitokea kikao cha bunge kilichopita. Nafikiri kulikuwa na bado kuna hoja nyingine nzito na nyeti zaidi ya hiyo ambazo zilistahili na bado zinastahili mjadala.

Monday, April 9, 2007

Pozi lake lina mvuto!

Moja ya hazina kubwa ya taifa. Anaonekana kama anasema "ok. nipo tayari nipige picha". Pundamilia huyu ni moja ya vivutio vingi vilivyo katika hifadhi ya taifa ya Ngorongoro Crater. Katika karne hii ya sayansi na teknolojia ni muhimu kuvitangaza vivutio hivi. Kama ilivyo habari, biashara pia ni kutangaziana!

Waweza usiamini, ila ndo ukweli!

Pichani ni makazi ya watu katika mji wa Nashville-TN. Picha nyingi kutoka nchi zilizoendelea huwa ni za kuonyesha mazuri il-hali kutoka Afrika ni za kuonyesha mabaya. Anyway, ninachotaka kukiwakilisha hapa ni kwamba si kila kitu ni shwari katika nchi zilizoendelea kama hii picha ya makazi ya watu katika mji wa Nashville-U.S inavyothibitisha.

Sunday, April 8, 2007

Yupi bora, Raisi mzee au kijana?

Raisi Abdulwaye Wade wa Senegal. Staili yake ya kunyoa ni ya kipekee miongoni mwa viongozi wa juu.

Friday, April 6, 2007

Maadhimisho ya mauaji ya mwaka 1994 nchini Rwanda.




Mauaji yaliyotokea nchini Rwanda mwaka 1994 kamwe hayatasahaulika. Si kwa wanyarwanda tu bali hata kwa wapenda amani kote duniani ingawa leo ni miaka 13 tangu yalipotokea. Sababu kubwa ya mauaji ilikuwa ni tofauti za ukabila baina ya makabila makuu mawili yaani wahutu na watutsi. Wengi wa waliouwawa walikuwa ni watutsi na wahutu wachache. Zaidi ya watu 800,000 walipoteza maisha na miongoni mwao 500,000 walikuwa watutsi. (Pia inakadiriwa waliokufa walikuwa zaidi ya 1,000,000). Mauaji haya yalifanywa na vikundi vya wanamgambo wa Kihutu maarufu kama Interahamwe na Impuzamugambi. Zilikuwa takribani siku 100 za umwagikaji wa damu usio na mfano kuanzia April 6 mpaka katikati ya mwezi wa saba. Lakini katika kuadhimisha siku hii hatuna budi kuungana na wenzetu wa Rwanda katika kudumisha udugu,mshikamano na umoja bila kujali tofauti za ukabila,udini na za kisiasa kwani tofauti katika nyanja hizi aghalabu ndio chanzo cha mifarakano miongoni mwa wanajamii. Hongera serikali ya Rwanda kwa mwanzo mzuri wa kuijenga Rwanda mpya yenye uchumi unaokua, miundo mbinu bora na pia huduma bora za kijamii.

Wednesday, April 4, 2007

Nyota yake iling'ara tokea akiwa bado kinda.

Vipaji (talents) mara nyingi huonekana tokea utotoni. Franco akiwa na miaka 7 alifanikiwa kutengeneza gitaa kwa kutumia lililokuwa kopo la bati la kuhifadhia mafuta ya kupikia. Alilitumia gitaa hilo kutoa burudani kwenye mechi za kandanda. Alifanikiwa kupata gitaa halisi alipokuwa na umri wa miaka 11. Wakati huo alikuwa kama mpiga gitaa wa muda tu katika studio ya Loningisa iliyokuwa ikimilikiwa na Wagiriki huko nchini Zaire. Kipindi hicho, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ilikuwa chini ya utawala wa Ubelgiji. Mwaka 1956, Makiadi alifanikiwa rasmi kuanzisha bendi ya OK Jazz ambayo baadaye ilikuja kujulikana kama TPOK Jazz. Aliongeza "TP=Tout Puissant" yenye maana ya "wote wana nguvu". Tizama moja ya kazi zake hapa.

Alipata kuitwa "Baba wa muziki wa Afrika". Ni Franco Luambo Makiadi!

Franco Makiadi alipata kuitwa baba wa muziki wa Afrika. Serikali ya Zaire ilimtunuku heshima ya "Grande MaƮtre", heshima ambayo ilikuwa mahsusi kwa majaji na wasomi. Pamoja na hayo, Franco aliwahi kufungwa na pia kuzuiliwa kutoka nje ya nchi kwa sababu ya ujumbe uliokuwa kwenye baadhi ya nyimbo zake. Baada ya kuondolewa kizuizi, Luambo Makiadi alipata kufanya ziara ya kimuziki nchini Uingereza na Marekani katikati ya miaka ya 80.

Luambo Makiadi aliimba kwa kutumia lugha ya Lingala na ujumbe katika nyimbo zake ulihusu mambo ya kijamii. Staili yake ya kufikisha ujumbe ni ya kutumia mafumbo huku ikichagizwa na maelezo ya hapa na pale. Aghalabu, ujumbe katika nyimbo zake huwa umefichama. Alipata kuimba juu ya serikali, nasibu mbalimbali za maisha mathalani ugomvi kati ya wanandoa. Binafsi aliipenda kazi yake na kibao alichokipenda na kilichopata kuitikisa Africa na kumletea heshima kubwa ni "Mario". Kibao hiki kinaelezea mapenzi baina ya kijana msomi lakini mvivu (hohehahe) na mwanamama mtu mzima mwenye uhakika wa maisha. Hatimaye kijana alifukuzwa na mwanamama huyo kwa kuonekana ni mnyonyaji (mchunaji). Ama hakika kibao hiki kilitia fora ya mauzo na bado kinazidi kuuzika hadi hii leo.
Lwambo Makiadi alifariki mwaka 1989 na mazishi yake yalifanywa kuwa ya kiserikali na alipewa heshima zote za kitaifa chini ya Serikali ya Zaire enzi hizo Raisi akiwa hayati Mobutu Seseseko "Kuku wa Zebanga". Viongozi na wawakilishi mbalimbali wa kitaifa kutoka nchi za Kiafrika na Wazaire mamia kwa maelfu walijumuika jijini Kinshasa kutoa heshima zao za mwisho kwa Franco.Serikali ilitangaza mapumziko ya siku 4 na stesheni zote za redio zilikuwa zikiporomosha muziki wa Franco mchana kutwa na usiku kucha. Huyo ndiye hayati Franco Luambo Luazo Makiadi. Matunda yake ni mwanamuziki Madilu Multi System. Daima utakumbukwa.
R.I.P Franco Makiadi.

Tuesday, April 3, 2007

Kama vile ice-cream za Bakhresa!

Biashara ya kuuza barafu (ice-cream) ni maarufu sana katika jiji la Dar-es-Salaam. Pichani ni biashara kama hiyo katika jiji la New York. Kwa ujumla mazingira ya biashara hii jijini NY yanafanana kabisa na yale ya jijini Dar-es-Salaam.

Friday, March 2, 2007

Yangehifadhiwa kuliko kutapishwa!

Ama hakika Mungu mkubwa! Kutoka kupungua kwa kina cha maji hadi kutapishwa kwa maji katika bwawa la Mtera. Ashukuriwe kwa hilo. Ndio hivyo maji yamejaa pomoni na mamlaka husika imeamua kutapisha maji toka mabwawa ya Mtera na Kidatu. Hakuna atakayesahau uhaba wa umeme uliolikumba taifa mwaka jana. Chanzo cha tatizo kilikuwa ni kupungua kwa maji katika bwawa la Mtera. Leo bwawa limejaa kwa uwezo wake Allah, cha ajabu maji yanatapishwa badala ya kubuniwa njia mbadala za kuyahifadhi kwa ajili ya matumizi ya baadaye endapo yatapungua. Baadhi ya nchi zina utaratibu wa kuhifadhi kwa ajili ya matumizi mbalimbali. Mathalani Misri ipo Jangwani lakini kwa kutumia maji ya mto Nile wameweza kuhifadhi maji ya kutosha. Kwa maana hiyo hata mto Nile ukikauka hii leo, bado watu wa Misri watakuwa na uhakika wa kupata maji. Tanzania tungeiga mfano wa nchi ya Misri. Kimsingi hakuna sababu ya kumwaga maji yaliyozidi katika mabwawa ya Mtera na Kidatu na badala yake mamlaka husika zingebuni utaratibu wa kuyahifadhi maji hayo kwa ajili ya akiba ili siku zijazo ikitokea yamepungua iwe rahisi kuyatumia pasi kusubiri mvua. Tujifunze kupitia makosa kwani hatuna mkataba na Mungu kwamba mvua itakuwa ya kutosha kila mwaka.

Kuna ulazima wanja jipya kuzinduliwa na Real Madrid?


Pengine kusimama kwa uwanja mpya wa michezo ni miongoni mwa mambo yatayotufanya watanzania tusiisahau serikali ya awamu ya tatu. Tayari maandalizi ya ufunguzi wa kiwanja hicho cha michezo yanazidi kushika kasi. Real Madrid moja ya timu kubwa tena tajiri pengine kuliko vilabu vingine duniani imekubali kushiriki sherehe za uzinduzi wa uwanja huu kwa kutoa masharti magumu ikiwa ni pamoja na kupatiwa tiketi za ndege kwa ajili ya msafara wa watu 80 (round trip) kutoka Dar hadi Madrid-Hispania. Japo mwaliko huo ulitolewa na serikali na pia gharama zote zitalipwa na serikali bado hakukuwa na ulazima sana wa kujiingiza katika gharama kubwa kwa ajili ya timu moja (Real Madrid). Ingependeza kama zingealikwa timu za taifa kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika kama vile Togo, Nigeria, Afrika ya Kusini, Misri n.k. Hii ingetosha kabisa kuchagiza sherehe za ufunguzi wa uwanja mpya. Lakini pia ingekuwa ni manufaa makubwa katika kuijenga timu yetu ya taifa kimazoezi kwa kucheza na timu za taifa kutoka mataifa mbalimbali. Wewe unasemaje?

Chuo Kikuu cha New York kuwa na tawi Tanzania, chatengewa ekari 500!

Waziri wa Mali asili na utalii Prof. J4 Maghembe akiteta jambo na wadau wa Chuo kikuu cha New York ikiwa ni jitihada za serikali ya awamu ya nne kuitangaza Tanzania na vivutio mbalimbali vilivyopo nchini. Wadau wa Chuo kikuu cha New York wameonyesha dhamira ya kufungua tawi la chuo hicho nchini Tanzania. Serikali imekipatia chuo hicho ekari 500 kwa ajili ya kufungua tawi hilo ambalo litaitwa NYU in Tanzania. Akiwa chuoni hapo Waziri wa mali asili na utalii aliwahakikishia uwepo wa eneo hilo. Hiyo ilikuwa tarehe 22/2/ 07. Chuo kikuu cha New York tayari kina matawi nchini Brazil, Canada,Uingereza na Ghana. Huenda Tanzania ikaingia kwenye hiyo orodha.

Friday, February 23, 2007

Kinyang'anyiro cha Urais wa Marekani 2008, Obama kufurukuta?


Seneta Barack Husein Obama moja ya wanaotajwa kumrithi Bush akitangaza azma yake ya kuwania nafasi hiyo.
Ni uchaguzi unaovuta hisia si tu za wamarekani bali pia watu wa mataifa mbalimbali duniani kote. Kinadharia inaonekana kama vile Democratic watashinda uchaguzi huo kwa vile ndicho kinacholidhibiti baraza la Congress. Lakini pia suala la vita nchini Iraq limekipunguzia umaarufu chama cha Republican. Ndani ya Democratic kuna pilikapilika za kuwania kuteuliwa kwa ajili ya kukiwakilisha chama katika uchaguzi huo. Wanaotajwa sana ni Seneta Barack Obama na Hilary Clinton mke wa Bill Clinton. Je uraisi wa Marekani kuendelea kuwa mikononi mwa familia mbili yaani familia ya Bush na Clinton iwapo Hilary atapitishwa? Ni swali linalotokana na baadhi ya vikwazo anavyowekewa Barack Obama. Baadhi ya watu wanalifananisha jina la Obama kama Osama na pia Husein kama lile la Saddam. Wengine wanaenda mbali zaidi ya kwamba kwa vile yeye ni mweusi asitegemee kitu japo watu wanamkubali. Zaidi ya hayo Barack Obama anasemekana alipata kusoma nchini Afghanistan na kwa maana hiyo wanamuona kama mtu anayeweza kuimarisha urafiki kati ya Marekani na nchi za kiarabu. Kipyenga ndio hivyo kimelia na sisi yetu macho. Nani kumrithi Bush? Mweusi au mweupe? Tusubiri!!

Friday, February 16, 2007

Wataiva lakini kwa mwezi moja?

Mh. Waziri mkuu ndugu Edward Lowasa.

Serikali kupitia Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari imefanikiwa kuanzisha shule nyingi za sekondari. Jambo hilo halikwenda sanjari na maandalizi ya walimu. Ili kukidhi matakwa Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Mh. Magreth Sitta amebainisha kuwa zaidi ya walimu 9000 wanahitajika. Tayari walimu 3,124 waliohitimu (mwezi mmoja) kabla ya muda wao wataajiriwa moja kwa moja na serikali pamoja na wengine 250 waliokuwa wamestaafu watarejeshwa kazini. Nafasi 6,000 zitajazwa na waliomaliza kidato cha sita ambao watapigwa msasa wa mafunzo ya ualimu kwa muda wa mwezi moja. Mwombaji anatakiwa awe na alama mbili za kufaulu mtihani wa kidato cha sita na baada ya mwezi moja atakuwa mwalimu wa sekondari. Inahitajika miujiza itakayomfanya muhitimu wa kidato cha sita kuwa mwalimu bora kwa kipindi cha mwezi mmoja. Kimsingi kozi ya ualimu ina mambo mengi na inatakiwa isiwe pungufu ya miaka miwili. lngawa serikali inahitaji walimu wengi na kwa haraka, njia hii ina walakini kama kweli itatoa walimu bora au bora walimu.

Gari linapokwama kwenye tope la theluji!

Wakati tatizo kubwa katika nchi yetu ni barabara mbovu zinazosababisha magari kukwama, kwa wenzetu hali huwa tete katika msimu wa barafu. Barabara nyingi huwa zimefunikwa na tope la barafu kama inavyoonekana pichani. Huo ni mtaa wa Chuo kikuu cha New York.

Hakatizi mtu hapa!

Beki mahiri wa timu ya soka ya taifa (taifa stars), Shadrak Nsajigwa akiumiliki mpira mbele ya mchezaji wa Tigres du Brasil katika moja ya mechi za kujiandaa kabla ya kukabiliana na Senegal. Katika mechi hiyo Stars ilala kwa bao 1-0.

Saturday, February 10, 2007

Tunakuamkua Abraham Lincoln!


Tukiwa katika makumbusho ya Rais wa 16 wa Marekani Bw. Abraham Lincoln jijini Washington D.C.
George Washington (1789-1797) ndio mtu wa kwanza kula kiapo cha kuwa raisi wa Marekani akiongoza mlolongo wa watu 43. Miongoni mwa watu 43, kuna ambao kamwe hawatasahaulika kwa namna walivyoliongoza vyema taifa hilo lenye nguvu kubwa kiuchumi na kidola. Majina kama Abraham Lincoln (1861-1865), Theodore Roosevelt (1901-1909), John Kenedy (1961-1963) n.k ni miongoni mwa waliopata mafanikio makubwa katika nafasi hiyo ya uraisi. Kama ilivyo kwa msemo wa kiswahili "vizuri havidumu" Lincoln pamoja na kuwa kiongozi makini aliuwawa kwa kupigwa risasi na mtu aliyejulikana kwa jina la John Wilkes Booth. Hiyo ilikuwa Aprili, 14 1865 baada ya baadhi ya watu kutoridhishwa na sera zake za kuutokomeza ubaguzi na kuwatetea weusi ili kuleta usawa miongoni mwa raia aliokuwa akiwaongoza. Huyo ndio marehemu Lincoln, Raisi wa 16 wa Marekani 1861-1865.

Baada ya pindua pindua Dar, Bonde la ufa-RVF laitikisa Arusha.

"Imepimwa hii na kuthibitishwa na mganga kuwa haina RVF". Nahisi ndivyo asemavyo huyu muuzaji wa duka la nyama jijini Dar es Salaam.


Ni ugonjwa ambao huikumba mifugo hususan iliyo katika bonde la ufa na hii ndio sababu hasa ya kupewa jina hili. Binafsi natoka katika jamii ya wafugaji na ugonjwa ambao niliwahi kushuhudia madhara yake kwa binadamu ni kimeta. Nilishuhudia watoto wawili wa familia moja wakipoteza maisha na watu wengine watano wa familia hiyohiyo wakiponea chupuchupu kupoteza maisha kwa kula nyama ya ng'ombe aliyekuwa na kimeta. Kwa ujumla magonjwa haya ya mifugo aghalabu huwa mwiba na tishio siyo tu kwa maisha bali hata biashara. Kwa kawaida watu wengi katika kipindi hiki huwa wanakuwa makini katika kutumia mazao yatokanayo na mifugo. Lakini kuna wengine wachache ama kwa kutoelewa madhara yake au kwa kufanya makusudi hujikuta wakiathirika vibaya na kupoteza maisha kwa kuyatumia mazao ya mifugo athirika. Tayari serikali imeisha toa tamko kupitia mawaziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Prof. David Mwakyusa na yule wa Maendeleo ya Mifugo Mh. Anthony Diallo wakiwatahadharisha wananchi kuwa waangalifu wakati wa kula nyama na mazao yote yatokanayo na ng’ombe, mbuzi, nguruwe na kondoo. Ugonjwa huu wa bonde la ufa umejikita Arusha ukitokea nchini Kenya. Jambo la msingi hapa kujiuliza ni je huko vijijini ambako ndiko hasa kwenye wafugaji wengi kuna wataalamu wa mifugo wa kutosha na kama wapo wana vitendea kazi vya uhakika? Sijui maana kijijini kwangu mganga wa mifugo ni moja na anahudumia zaidi ya vijiji vitatu. Zemarcopolo nipo kwenye anga zako, tujadiliane.

Friday, February 9, 2007

Kama vile wanaimba "kama siyo juhudi zako Nyerere, CCM wangesoma wapiiii"


Wanafunzi wa taasisi za elimu ya juu wakijumuika na wana-CCM wengine katika kusheherekea miaka 30 tangu kuzaliwa kwa chama hicho ndani ya ukumbi wa Diamond Jubilee.
Ni kama vile walijisahau na badala ya kusheherekea miaka 30 ya kuzaliwa kwa chama tawala (CCM), wanafunzi toka vyuo vya elimu ya juu walimtaka mwenyekiti wa chama taifa ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano Mh. JK atoe msimamo wa serikali kuhusu wanafunzi wa taasisi hizo kuchangia 40% ya karo zao. Hakika majibu ya mheshimiwa Rais yalipokelewa kwa furaha pale aliposema serikali yake italiangalia upya suala hili. Kwa ujumla unapoongelea maendeleo ya taifa lolote hapa duniani ni nadra sana kutokuhusisha wasomi wa taifa hilo. Kimsingi wasomi kutoka taasisi za elimu ya juu ndio wataalamu wa kufanya tafiti mbalimbali kwa ajili ya kuchochea maendeleo. Kwa ufupi 40% kwa mtanzania mwenye kipato cha chini ni mzigo usiobebeka na kama hivyo ndivyo na msimamo wa serikali ukabaki kama ulivyo kuna uwezekano mkubwa kwa vijana wengi kushindwa kuendelea na masomo ya juu. Hii maana yake ni kwamba tabaka kati ya walio nacho na wale wasio nacho litazidi kuongezeka huku maendeleo ya nchi kwa ujumla yakizidi kudidimia. Ni vema suala hili likaangaliwa upya kama alivyosema kiongozi wa nchi. Elimu kama chachu ya maendeleo haina budi kutolewa bila vikwazo.

Thursday, February 8, 2007

Heshima nyingine kubwa kwa nchi yetu.

Baadhi ya wanajeshi wa Jeshi la Ulinzi Tanzania (JWTZ) wanaokwenda kulinda amani nchini Lebanon. Picha na Richard Mwaikenda.

Tanzania imepeleka jumla ya wanajeshi 80 wa Jeshi la Ulinzi Tanzania (JWTZ), kwenda nchini Lebanon kushiriki kulinda amani wakiwa ni sehemu ya vikosi vya Umoja wa Mataifa. Hii pia ni sifa nyingine kwa nchi yetu ikizingatiwa kuwa naibu katibu mkuu wa umoja wa mataifa (UN) pia anatoka Tanzania. Cha msingi ni kwamba askari hao ambao kati yao 11 ni wanawake, kuiwakilisha vyema nchi yetu kwa kuwa na nidhamu na kujiepusha na vitendo vya utovu wa nidhamu kama jeshi linavyoelekeza. Ama hakika hii itakuwa ni nafasi nzuri kuonyesha kwa vitendo yale waliyojifunza na pia kujifunza mengine watakayoyakuta huko kwenye operesheni ya kulinda amani. Mara ya mwisho Tanzania ilitoa askari wake kwenda kulinda amani katika mpango kama huo nchini Liberia kati ya mwaka 1993 na 1995. Mungu ibariki Tanzania na wanajeshi wetu huko Lebanon.

Wednesday, February 7, 2007

Kwa kasi hii Simba wa Teranga wajizatiti!!

Wachezaji wa timu ya soka ya Taifa (Taifa stars) al-maarufu kama "JK boys" wakiwa mazoezini katika kituo cha mafunzo ya michezo cha Fluminense jijini Rio de Janeiro Brazil. Kutoka shoto ni Mwaikimba, Nsajigwa, Maulid & Yusuf. Picha na Benny Kisaka.

Katika dunia hii hakuna lisilowezekana. Waingereza wana msemo wao "nothing imposible under the sun" wakimaanisha hakuna kisichowezekana hapa duniani. Kama hivi ndivyo, bila shaka hakuna kitakachoishinda timu ya taifa ya kabumbu kufanya kile kinachosubiriwa kwa shauku kubwa na mamilioni ya wapenda kandanda kote nchini. Ikiwa inaongoza katika kundi lake, maendeleo ya timu si mabaya na kwa muda wa mwezi moja itakuwa nchini Brazil kwa ajili ya kujifua kabla ya kucheza na Senegal moja ya nchi zilizopata mafanikio makubwa katika mchezo wa mpira wa miguu barani Afrika. Lakini hicho si kikwazo cha kuifanya timu yetu iwe imefungwa hata kabla ya mchezo. Chini ya mwalimu Maximo toka Brazil nchi ambayo kiwango chake katika mchezo huu ni cha hali ya juu, wachezaji wote wanayapokea mafunzo yake vizuri na wanajituma katika kufanya mazoezi kama inavyotakiwa na tena kwa moyo mkunjufu. Serikali ilitoa tamko ya kwamba haitavumilia vitendo vya utovu wa nidhamu katika kambi hiyo na pia ni jukumu la wachezaji wote kuwa na moyo wa uzalendo. Kwa ufupi ni kwamba mtanange kati ya Stars na Simba wa Teranga itajumuisha wanaume 22 kwa uwiano wa wachezaji 11 toka kila upande. Haogopwi mtu hapa! si Diof, Camara wala Diop. Ni mabao tu toka kwa Mwaikimba, Maulidi na Maftah. Mungu ibariki Stars, Mungu ibariki Tanzania.

Monday, February 5, 2007

Kiswahili nacho kilitumika kuwakilisha.

Waalimu andamizi wa lugha toka nchini Tanzania wakiwakilisha kwa kutumia lugha ya kiswahili katika kongamano la walimu mbalimbali wa lugha lililofanyika San Diego huko Califonia. Toka kushoto ni Mwl. Juma Binagirioba (Bowling Green University) na Mwl. Zablon Mgonja (Fisk University).
Lugha ni chombo muhimu cha mawasiliano. Kama zilivyo lugha nyingine, kiswahili kwa sasa kinazidi kupata umaarufu si Afrika tu bali hata nje ya Afrika kama vile Amerika na Ulaya. Mathalani vyuo vingi nchini Marekani vimeanzisha idara za kiswahili ambapo wanafunzi wengi wanajiandikisha kwa ajili ya kujifunza lugha hii. Kama ilivyo kwa mlima Kilimanjaro, pia wamarekani wengi wanaamini ya kwamba kiswahili sanifu kinazungumzwa nchini Kenya. Kutokana na imani hiyo hata walimu wengi wanaofundisha kiswahili katika vyuo hivyo wanatoka nchini Kenya. Pamoja na hayo walimu wachache toka Tanzania wamepata umaarufu mkubwa na ufanisi wa hali ya juu kwa muda mfupi walioutumia kufundisha. Kimsingi katika bara la Afrika kiswahili sanifu kinazungumzwa nchini Tanzania. Tatizo hapa ni kwamba kuna mapungufu katika kuitangaza Tanzania yetu, lugha yetu ya kiswahili pamoja na vivutio lukuki tulivyonavyo. Kuna msemo usemao "usipozungumza hautajulikana kama upo" . Kwa msemo huu ni muda muhali sasa kuitangaza nchi yetu.

Saturday, February 3, 2007

Tutaamka kikieleweka!!!

Ni kupumzika tu muda wowote na mahala popote. Picha kutoka darhotwire.

Ni wimbo ambao unatia fora karibu ulimwenguni kote. Wimbo wenyewe si mwingine bali ni ule uliopo kwenye albamu ya siku nyingi ya uchumi unaokwenda kwa jina la ajira. Kwa nchi zilizoendelea (za dunia ya kwanza) wimbo huu si maarufu sana. Kwa upande wa nchi zinazoendelea, wimbo huu ama hakika unatikisa vilivyo kila uchao. Nchi yetu kama zilivyo nchi nyingine zinazoendelea inajitoa muhanga kwa kufanya kila linalowezekana kupunguza idadi ya wananchi hususani vijana wanaoimba kibao hiki japo kimepitwa na wakati ikizingatiwa ni karibu miaka 45 tokea nchi yetu ipate uhuru. Katika kufanikisha uwezeshaji kwa wananchi, serikali ya awamu ya nne chini ya Mh. Raisi J.Kikwete imeisha toa shilingi bilioni 1 kwa kila mkoa. Kwa ujumla ni mwanzo mzuri kama kutakuwa na usimamizi mzuri na masharti nafuu ili kuwawezesha walengwa haswaa kupatiwa mkopo huo. Vile vile ni wakati mzuri pia kwa benki zetu na asasi binafsi kuangalia uwezekano wa kutoa mikopo kwa wananchi ili kuchagiza mchakato mzima wa kuwawezesha wananchi kujiajiri wenyewe. Kama haya yote yatafanyika na mazingira mazuri yataandaliwa bila shaka hata waliolala wataamka. Namalizia kwa kusema "kama wao wameweza wana nini na sisi tushindwe tuna nini?"

Thursday, February 1, 2007

Rada, moto uliozimika na kulipuka tena.

Mh. JK Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akifafanua jambo kuhusu mustakabali wa Taifa letu.

Kwa kile kilichoelezwa kuwa ni harakati za kiusalama, serikali ya Tanzania mnamo mwaka 2002 ilitumia karibu Tshs bilioni 50 kwa ajili ya manunuzi ya Rada toka kwa serikali ya Uingereza kupitia shirika la BAE System. Mengi yalisemwa na watanzania wakati wa mchakato mzima wa suala la ununuzi wa rada na hatimaye yakasahaulika hadi mwaka huu baada ya wabunge wa Uingereza kuihoji serikali yao kwa kile kinachoonekana kuwa haikutenda haki kuiuzia Tanzania chombo hicho ambacho si cha kisasa tena kwa bei ya juu. Hivi sasa suala hilo kwa upande wa Uingereza limeachiwa Kitengo cha Kupambana na Makosa ya Ulaghai (SFO) ili kuchunguza madai kuwa kampuni ya BAE Systerm iliiuza rada hiyo kwa bei ya juu tofauti na bei halisi na pia kama ilitoa kamisheni ya sh. bilioni 12 kwa mtu aliyefanikisha ununuzi huo. Wakati hali ikiwa hivyo huko Uingereza, kwa upande wa Tanzania tayari yaliishafanyika maandamano kulaani ununuzi wa chombo hicho. Serikali imesisitiza kwamba inasubiri ripoti kutoka Uingereza ili kujua kama kuna watanzania waliohusika katika kashfa hiyo. Katika kulizungumzia sakata hilo serikali imesisitiza iwapo uchunguzi utabaini ya kwamba Tanzania ilidhulumiwa, kuna uwezekano mkubwa itatuma maombi kwa Serikali ya Uingereza ili kudai fedha zilizozidi. "Rada moto uliozimika na kulipuka upya".

Tuesday, January 30, 2007

Ni shule mtindo mmoja bila kujali umekalia kiti au umekaa chini.

Hali inavyokuwa wakati wa muhadhara katika moja ya kumbi za mihadhara chuo kikuu Mlimani.

Chuo kikuu cha Dar es Salaam pengine ndio taasisi kubwa ya elimu ya juu kuliko taasisi nyingine zote. Si tu ni taasisi kubwa kwa kuwa na muda mrefu tokea kuanzishwa, bali pia ndiyo taasisi pekee inayodahiri idadi kubwa ya wanafunzi kwa ajili ya stashahada, shahada, na shahada za uzamili. Taasisi hii kwa sasa inakabiliwa na changamoto lukuki ikiwa ni pamoja na uwiano usiokuwa sawia baina ya idadi ya wanafunzi na vitendea kazi kwa ujumla wake. Mathalani kumbi za mihadhara zilizojengwa kwa ajili ya kupokea wanafunzi 400, kwa sasa zinalazimika kutumiwa na wanafunzi zaidi ya 1000. Katika nadharia ya kweli ili mwanafunzi aelewe vizuri kile anachofunzwa anapaswa kuwa katika mazingira mazuri huku akili ikiwa imetulia. Lakini kwa chuo chetu hiki hali ni tofauti maana muda mwingi mwanafunzi anawaza kama kipindi kijacho utapata kiti au utaketi chini tena. Ndio hivyo kwa mazingira hayo hayo watu wanahitimu kila mwaka. Ni wakati sasa kwa uongozi wa chuo kwa kushirikiana na serikali yetu kuyabadili mazingira ya chuo ili kiwe na hadhi ya chuo kikuu. "Elimu ndio ufunguo wa maendeleo".



Vivutio si kwa ajili ya wageni tu, hata wazalendo tunaweza kuwa watalii.

(Pichani watanzania waishio Moshi walioamua kutembelea vivutio mbalimbali kama bango linavyojionyesha. Picha kwa hisani ya Juma Iddi Issa -wa kwanza toka kushoto.)

Tanzania yetu imejaliwa kuwa na vivutio vingi kama vile mbuga za wanyama, mabonde mazuri ya kuvutia, mlima mrefu wa Kilimanjaro, maziwa na mito mingi karibu kila kona ya nchi. Lakini wageni toka nje ya nchi ndio kwa asilimia kubwa wanaovitembelea vivutio hivyo ikilinganishwa na wazawa. Binafsi naweza sema ni kasumba ambayo wazalendo tumejijengea ya kwamba vivutio hivi ni kwa ajili ya wageni (watalii). Kimsingi si wanaotoka nje tu ndio wanapaswa kuwa watalii bali hata sisi watanzania tunaweza kabisa kuwa watalii kwenye vivutio mbalimbali ndani ya nchi yetu. Cha msingi hapa ni serikali kupunguza viingilio kwa wazawa ili kutoa nafasi kubwa kwa wananchi bila kujali vipato vyao. Ni aibu mtu kutoka Amerika ya kusini au Mashariki ya mbali na kuuetembelea mlima Kilimanjaro ili hali mimi na wewe tuliozaliwa na kukulia Tanzania si tu hatujawahi kuutembelea bali hata historia yake hatuijui vizuri. "Nakupenda Tanzania"

Sunday, January 28, 2007

Uzalendo upewe kipaumbele badala ya unazi!

Wawakilishi wa Tanzania ktk ligi ya mabingwa Afrika-Yanga kabla ya ushindi mnono wa 5-1 dhidi ya AJSM ya Comoro. (Picha kwa hisani ya Muhidin Michuzi)
Moja ya sera za serikali ya awamu ya nne chini ya Mh. JK ni kuinua michezo na kwa kuanza mchezo wa mpira wa miguu maarufu kama kandanda ndio umepewa kipaumbele.Kutambulika kwa nchi yetu katika ramani ya kabumbu barani Afrika na ulimwenguni kwa ujumla kutatokana na kuimarika kwa vilabu vyetu.Ili kuwa na timu nzuri ya taifa ni vizuri tukawa na vilabu bora vyenye kufanya vizuri katika mashindano ya kimataifa. Kwa ujumla Yanga na Simba ndio vilabu vikubwa katika soka nchini Tanzania vinavyovuta hisia za mashabiki lukuki. Kuwa mnazi wa Simba au Yanga ni utashi lakini ni vema jambo hili likaenda sanjari na uzalendo unapofika wakati wa mechi za kimataifa. Mathalani mwaka huu Yanga ndio wawakilishi wa nchi yetu katika ligi ya mabingwa Afrika ili-hali Simba ni wawakilishi katika kombe la CUF. Kimsingi umefika wakati sasa kwa mashabiki wa timu za Yanga na Simba kuuvaa uzalendo na kuondoa tofauti za kiushabiki wakati moja ya timu zetu inapokuwa inaliwakilisha taifa letu. Mechi za uwanja wa nyumbani ni mechi muhimu ambazo ni vizuri timu zetu zikazitumia kuvuna ushindi mnono.Kisaikolojia mashabiki wana nafasi yao katika kufanikisha au kuzorotesha ushindi ama kwa kushangilia au kwa kuzomea.Si vema na wala si busara kwa watazamaji wanaoingia uwanja wa taifa kutowashangilia wawakilishi wetu kwa kisingizio cha unazi wa Yanga na Simba. Kwa ujumla timu zetu za Yanga na Simba zina nia na uwezo wa kulitoa kimasomaso taifa letu katika mechi za kimataifa.Wanazi tutoe ushirikiano wa kutosha. Mungu Ibariki Tanzania.

Saturday, January 27, 2007

Nembo za taifa kielelezo cha uzalendo,sheria iruhusu zitumike.


Ama hakika rangi za bendera yetu zinapendeza.
Bendera ni miongoni mwa nembo za taifa na pia ni kitu cha kujivunia kwa kila mwananchi. Kimsingi bendera ni alama ya utaifa na pia ni kielelezo halisi cha uzalendo.Umefika wakati sasa iwe ni ruhusa kwa wananchi kuitumia bendera ya taifa kwani bendera ya taifa ya nchi ndio utambulisho wa nchi na kwa mtu yeyote mzalendo anapoiona bendera ya taifa lake ikipepea mahali fulani, hupata mvuto wa kipekee na pia hukumbuka nyumbani.Mathalani kipindi hiki cha kuinua kandanda Tanzania ni vema ikawa ni ruhusa kwa rangi za bendera kutumiwa na watanzania katika kuishangilia timu ya taifa ya soka na hata timu za taifa za michezo mingine.Vile vile iwe ruhusa kwa watanzania kushona na kununua nguo zenye rangi ya bendera ya taifa tofauti na sasa ambapo watanzania tunabanwa na sheria ya nchi.Mathalani katika mataifa kama Uingereza au Marekani, ni rahisi kukuta nguo, kofia, kalamu, vitambaa na hata makaratasi yenye rangi zinazoonyesha bandera ya nchi hizo yakiwa yamepamba mitaa ya miji. Ni muda muafaka kwa sheria za nchi yetu kufanyiwa marekebisho.Vinginevyo nchi yetu itaendelea kutotambulika na hali kadhalika sifa kemkem za nchi yetu kama vifutio vya utalii vitaendelea kutangazwa kuwa vipo nchini Kenya na wala si Tanzania. Mungu ibariki Tanzania.

Friday, January 26, 2007

Ukitembea utaona au kusikia mengi.

Pichani mwanadada akila pozi na mbwa wake.
Walipata kunena wahenga "ukishangaa ya Musa utayaona ya Firauni". Hawakuishia hapo pia waliibuka na msemo mwingine "tembea uone". Kwa ujumla hizi semi mbili zina maana kubwa iliyofichamana. Mwanamuziki wa kizazi kipya nchini Tanzania ana kibwagizo fulani cha "mbado".Niliwauliza maswali machache marafiki zangu waliopo Tanga na majibu yao yalikuwa mbado. Maswali yangu yalikuwa kama hivi:-
Mimi- Mmewahi kuona mbwa akipigwa busu?
Wao-mbado.
Mimi- Mmewahi kusikia mbwa akiitwa "he" au "she"?
Wao-mbado.
Mimi-mmewahi kusikia mbwa akilala chumba achilia mbali kitanda kimoja na binadamu?
Wao-mbado.
Mimi- jamani hamjayaona wala kuyasikia hayo yote?
Wao-mshangao!!-mbado.
Ndio hivyo hayo mambo yapo.Baada ya kutembea nilibahatika kujua kwamba hayo yote niya kawaida katika jamii za kimagharibi. Mathalani hapa Marekani mbwa hana nafasi kubwa katika suala zima la ulinzi bali ni rafiki mkubwa wa binadamu hali inayopelekea mnyama huyo apewe heshima kubwa na upendo wa hali ya juu. Kupigwa busu, kupewa heshima ya ubinadamu na hata kushea sehemu za kulala ni mambo ya kawaida anayofanyiwa mnyama huyu hapa Marekani. Baada ya kufanya udadisi wa hapa na pale kwa wenyeji wangu wa hapa, majibu niliyopata ni kwamba mnyama mbwa ni rafiki yao mkubwa kwa misingi ya kwamba huwa anawaondolea upweke wale wenye upweke na pia hutoa kampani kwa wasio kuwa na kampani. Bado kwangu imekuwa ngumu kuwaelewa wenzetu hawa na huu urafiki wao kwa hawa wanyama. Uchunguzi wangu usiokuwa rasmi sana unaonyesha wanaume wengi wanakuwa pamoja na mbwa jike na hali kadhalika wanawake wengi wana midume ya mbwa. Nimeiweka hii mada ili nipate maoni kutoka kwa yeyote anayejua lolote juu ya hili suala.

Tuesday, January 23, 2007

Kama ni koleo, basi liitwe koleo.

(Pichani mwenye batiki ni mke wa mwanaharakati mahiri kutoka Kenya aitwaye Ngugi wa Thiong'o. Wengine ni wanafunzi wa NYU kutoka nchini Tanzania na Kenya.)
Kwa umri nilionao nimepata kuyasikia maneno mbalimbali yakiwa na maana tofauti.Mengi ya maneno yasiyotamkika mbele ya hadhira nilikuwa nikiyasikia tu toka kwa wale wa rika langu bila kujali jinsia. Hakuna anayeweza kubisha kwamba wanapokutana watu wa rika moja si muda wote huwa wanakuwa serious, kuna wakati hali hubadilika na maneno mbadala hutumika ili kuchagiza story. (siwezi yataja hapa). Baada ya utangulizi huo,napenda kutoa shukrani zangu za dhati kabisa kwa mke wa Ngugi wa Thiong'o anayejulikana kama Nyeri wa Ngugi. Bila shaka unakumbuka mkasa uliowapata yeye na mme wake walipoitembelea Kenya mwaka 2005.Kama ilivyoripotiwa na vyombo vya habari, mama huyu mbele ya kadamnasi iliyokuwa imekusanyika katika ukumbi wa Silver Centre hapa New York University alibainisha ukweli na kwa kuyatumia maneno halisi kwamba walipovamiwa na majambazi licha ya kuporwa pia walitenganishwa vyumba na hatimaye wakamuingilia kwa nguvu (kumbaka). Akiendelea kufafanua anasema alikuwa anahofia sana kuambukizwa ukimwi na si vinginevyo.Lakini kwa taratibu za wanawake wa Kenya na Afrika kwa ujumla ni nadra sana kwa mtu aliyeolewa kusema amebakwa. Yawezekana ni kwa kuogopa talaka au aibu (mimi sijui). Sasa kutokana na hii tabia ndio maana ninadiriki kutoa shukrani kwa mama huyu aliye na umri zaidi ya mama yangu kwa kuwa muwazi na kuyatamka hadharani maswahibu yaliyompata. Hii ni changamoto kwa wanawake hasa walio kwenye ndoa ya kwamba "koleo ni lazima waliite koleo"

Monday, January 22, 2007

Upi muziki wa Tanzania?

Wahenga walinena "kazi na dawa".Ndivyo inavyojidhihirisha katika picha ambapo waafrika mbalimbali waliamua kuifurahia ladha ya taarabu wakati wa sherehe za kuanza muhula wa pili wa masomo hapa NYU. Sipo pichani,ila kabla ya hapo niliwapa shule kidogo namna ya kuicheza na hayo ndo matokeo yake.

Miongoni mwa maswali magumu nilowahi kuulizwa ni hili la kuhusu muziki wa Tanzania.Kwa sababu ilikuwa ni mkusanyiko wa Waafrika mbalimbali na wengi wao walikuwa kutoka Afrika magharib,msema chochote hakuchelewa kuniita na mara baada ya kunitambuza aliniuliza ni upi muziki ambao ni kielelezo cha Tanzania kiasi kwamba ukiusikia tu unajua huu ni kutoka Tanzania? Palikuwa hapatoshi lakini kwa vile nilikuwa na CD za taarabu ikabidi nimwambie ni "taarabu" ili kuepuka aibu ya kuiangusha nchi yangu miongoni mwa macho ya wageni wengine. Basi kutoka kwenye hiyo CD ya East Africa Melody kilipigwa kibao cha "viumbe wazito" na nika-demonstrate namna ya kuicheza taarabu kabla ya hadhira kunyanyuka na kuniunga mkono. Baada ya hizo dondoo chache narudi kwenye mada kuu kwamba upi hasa ndo muziki wa Tanzania? Nashindwa na sijui sawasawa kati ya mduara,taarabu,dansi,bongo flava, n.k ni upi ndo kielelezo cha muziki wa Tanzania. Dunia kwa hivi sasa imekuwa kijiji kimoja na kwa maana hiyo waweza kutumia lugha yoyote ile lakini bado uka-maintain muziki wa asili yako.Mfano halisi ni kundi la Mandinka toka Afrika magharib wana wimbo wao moja wenye maneno mengi ya kiswahili lakini bado ukiusikia unajua kabisa ni kutoka Afrika ya magharibi.Kwa anayejua anisaidie kunijuvya ni upi hasa ndo muziki wa Tanzania?




Wababe wa kivita.

Tukiwa mbele ya sanamu la mashujaa sambamba na "double M" mjini Washington DC.

Katika hali ya kawaida vita si lelemama na wala si suala la kuombea.Ukilinganisha kati ya faida na hasara za vita, haiyumkini hasara zitachukua asilimia kubwa kuliko faida.Pamoja na hayo kuna vita visivyoepukika na vipo vita vya kuepukika.Si lengo langu kujadili aina za vita. Kama picha inavyojieleza, hiyo ni sehemu maalum kwa ajili ya kutunza kumbukumbu ya mashujaa walioshiriki vita vya Vietnam.Nchi ya Marekani inawaenzi kwa namna ya kipekee mashujaa wao al-maarufu kama"wababe wa kivita".Nini somo kwa nchi yetu ambayo miaka ya 1978 ilijikuta katika vita dhidi ya nduli Idd Amin Dada? Binafsi naona umefika wakati sasa kwa serikali ya Tanzania kuwaenzi wapiganaji wetu (wababe wa kivita chini ya amiri jeshi mkuu hayati Mwl. Nyerere) kwa namna walivyojitoa muhanga na hatimaye kuinusuru sehemu ya ardhi ya nchi yetu iliyotaka kuporwa na Nduli. Tuwape heshima stahili wote waliopoteza maisha wakati wa vita na pia washiriki wote ambao bado wapo hai. Mathalani serikali inaweza ikawaenzi kwa kutoa 50% ya ada kwa watoto wa mashujaa walau katika shule za sekondari. Nategemea maoni mujarabu kutoka kwenu.

Thursday, January 18, 2007

Kandanda ni kipaji na elimu pia.

Pichani Mwl. Merchedes Method (katikati) aliye chuo kikuu cha Wisconsin akisikiliza kwa makini maelezo kutoka kwa kocha wa chuo (hayupo pichani) wakati wa mapumziko. Katika mechi hiyo Wisc. walishinda 2-0 huku yeye akiwa kapachika kimiani bao moja.
Wakati dunia hivi sasa inashuhudia maendeleo makubwa ya Sayansi na Teknolojia katika kila nyanja, soka la Tanzania limeendelea kutawaliwa na vibweka vinavyoashiria imani kali za kishirikina kama inavyokuwa wakati wa mpambano wa vigogo vya soka nchini Simba na Yanga.Umefika wakati sasa kuachana na imani hizo na kuwekeza katika rasilimali watu ili kuinua kiwango cha kabumbu la bongo.Tanzania imejaliwa vipaji vingi vya wachezaji. Mojawapo ya vipaji hivyo ni kijana Merchedes Method (double M) aliye katika chuo kikuu cha Wisconsin nchini Marekani. Licha ya kufundisha kiswahili chuoni hapo,pia amejijengea umaarufu mkubwa katika fani ya mpira wa miguu maarufu kama futibo.Amekuwa gumzo chuoni hapo kutokana na uwezo wake wa kumiliki mpira,kupangua misitu ya mabeki kwa chenga za maudhi na pia kwa mashuti yake mazito.Habari njema kwa Tanzania kwa ujumla ni kwamba kijana huyo pia anahudhuria mafunzo ya ukocha chuoni hapo.Tunamuomba akimaliza muda wake arejee nchini na kuboresha mchezo wa mpira wa miguu.

Monday, January 15, 2007

Dhana ya sadaka.

Muongozo wa dini ya kiislam.
Sadaka katika lugha rahisi ni kitu chochote kinachotolewa na mwenyenacho ili kumsaidia asiyekuwa nacho. Kiundani, mtu yoyote anaweza kutoa sadaka bila kujali kama ni tajiri au masikini. Inasemekana sadaka ya masikini ni bora zaidi kuliko sadaka ya tajiri.Sadaka inaweza ikawa chakula,mavazi,fedha n.k. Dini zote zimeweka wazi kwamba sadaka ni siri kiasi kwamba kama umeitoa kwa mkono wa kulia basi hata ule wa kushoto usijue kuwa mkono wa kulia umetoa nini.Kimsingi sadaka sio jambo la kutangaza kwa maana ya kwamba unapoitoa,unakuwa unamtolea Mungu naye anakuona.Kama utaitoa sadaka kwa minajili ya kujipatia umaarufu/ufahari ama hakika haiwezi pata baraka toka kwa Mungu.Maoni yangu ni kwamba sadaka zitolewe kama dini zetu zinavyoelekeza.

Friday, January 12, 2007

Hivi kweli taifa linakabiliwa na uhaba wa walimu?

(Pichani Mwl.Ngugi alipolitembelea darasa langu la kiswahili.Umefika wakati kwa serikali ya Tanzania kuwathamini walimu kwani walimu ni funguo za fani anuwai.)

Kama ambavyo haijulikani ni kipi kilitangulia kati ya kuku na yai,hali kadhalika na mimi sijui ni kipi kinatangulia kati ya elimu na maendeleo.Ninachoweza kusema, elimu ni chachu (catalyst) ya maendeleo.Elimu ni neno moja ambalo linabeba maana pana na inayojitosheleza.Wanazuoni mbalimbali walitoa nadharia zao juu ya neno hili.Mathalani Aristoto analifafanua neno elimu kama kitendo cha mtu kuweza kuyafahamu yale asiyokuwa akiyafahamu hapo awali.Aristoto anaendelea kuielezea elimu kama ni kitu ambacho kipo siku zote tangu siku mwanadamu anapozaliwa hadi siku ya kufa.Kimsingi elimu ni chachu ya maendeleo kwa jamii yoyote hapa duniani.
Ili kuweza kutoa elimu bora vinahitajika vitu vikuu vitatu; mosi - miundo mbinu kama vile vyumba vya madarasa, pili -walimu bora na tatu-vitendea kazi kwa ujumla wake.Kwa ujumla tatizo kubwa katika huo utatu ni ukosefu kama si upungufu wa walimu.Hili limekuwa tatizo lisilopatiwa ufumbuzi wa kudumu hapa nchini.Siyo shule za msingi wala sekondari au vyuo vikuu,muziki ni ule ule tu; yaani uhaba kama si upungufu wa walimu.
Ukiondoa miji mikubwa kama vile Dar es Salaam,Mwanza na Arusha na pengine katika kila makao makuu ya mikoa na wilaya ni mifano michache ya sehemu ambazo zinajitosheleza.Kwa upande mwingine hali ni mbaya katika maeneo mengine hususani vijijini. Mathalani shule za sekondari zimefunguliwa na zinaendelea kufunguliwa katika kila kata huku zikiwa hazina walimu wa kutosha na lau kama wapo basi ni chini ya idadi na viwango vinayotakiwa.
Kwa ujumla idadi ya walimu wanaohitimu mafunzo ya ualimu kwa ngazi ya stashahada na shahada ni ya kuridhisha na kama wote wakipatiwa mazingira mazuri ya kufanya kazi katika maeneo mbalimbali yenye upungufu hakika tatizo la upungufu wa walimu linaweza kupatiwa ufumbuzi wa kudumu.
Changamoto kwa wizara ya elimu na mafunzo kwa kushirikiana na wizara za sayansi teknolojia na elimu ya juu na ile inayoshughulikia masuala ya ajira waliangalie suala hili kwa mapana yake ili Tanzania iachane na wimbo wa ukosefu wa walimu katika shule za sekondari zinazomilikiwa na serikali pamoja na zile za wazazi kwa kutoa ajira kwa wahitimu wote wa fani hiyo ikiwa ni sambamba na maslahi mazuri kama zilivyo sekta nyingine hapa nchini. "Ualimu ni kazi bwana na wala sio wito".

Tuzithamini bidhaa za ndani.

(Pichani; Bidhaa za kigeni ambazo kimsingi tunakula ili tushibe. Mara nyingi vyakula hivi huwa havina ladha nzuri na asilia.)

Binadamu tunatofautiana kwa silka na hulka. Kila mtu ana tabia zake ambazo haiyumkini zaweza kuwa nzuri au mbaya pia. Binafsi naweza sema umaarufu ni moja ya sifa kubwa inayotafutwa kwa nguvu zote na asilia kubwa ya binadamu. Kuna haja gani ya kwenda kulinunua chenza toka Afrika ya Kusini lenye ubora sawa na lile linalotoka Muheza kwa bei ya juu? Hainingii akilini na ndio maana naona kama huo ni utafutaji tu wa umaarufu.
Kwa bidhaa za mashambani Tanzania tumejaliwa (endowed) aina mbalimbali za vyakula vilivyo na ubora wa kutosha.Mathalani kuna machungwa yanaozea mitini huko Muheza,kuna milima kama si vifusi vya mananasi pale Chalinze,kuna ndizi nyingi huko Tukuyu,Mlimba na Bukoba.Viazi pia vipo vya kutosha huko Njombe na Morogoro.Nyanya zinapatikana kwa wingi Iringa na Morogoro.Hiyo ni mifano michache tu.Pamoja na uwingi wa bidhaa bora toka ndani ya nchi, haiyumkini bado kuna hizi zinazoitwa "Shopping centres" mijini zenye kuuza bidhaa za kigeni za mashambani kama vile matunda kutoka nchini Afrika ya Kusini tena kwa bei ya juu. Umefika wakati sasa kwa walaji kubadilika na kuondoa dhana iliyojengeka miongoni mwetu kwamba kila kinachotoka ng'ambo ni bora.Sambamba na hilo kuna haja ya kuboresha mazingira na kukuza soko la bidhaa za ndani kwa minajili ya kuwanusuru wakulima na wazalishaji wa ndani na pia kukuza pato la taifa.Kwa ufupi linahitajika soko madhubuti na mipango endelevu kwa ajili ya bidhaa za ndani.Tusipokuwa makini kuna siku maduka haya makubwa yatatuuzia chapati zilizookwa Afrika ya Kusini na Uarabuni.